Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Bodi ya Huduma za Maktaba Tanzania

TLSB Logo TLSB Logo
Tafuta kwenye kwa
VIJANA WATAKIWA KUTUMIA AKILI UNDE KUKUZA TALANTA ZAO
20 Nov, 2025
service image
Vijana nchini wametakiwa kujenga mazoea ya kutumia maktaba katika enzi hii ya mabadiliko na kukua kwa teknolojia hasa Akili Unde, ili kujiongezea ujuzi unaohitajika katika dunia ya sasa. Hayo yamesemwa tarehe 19 Novemba, 2025 na Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya huduma za Maktaba Tanzania, Dkt. Mboni Ruzegea katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa TLSB, Posta Dar e Salaam ikiwa ni maandalizi ya kuelekea Maonesho ya 32 ya Vitabu ya Kimataifa Tanzania yaliyoandaliwa na Chama cha Wachapishaji Tanzania (PATA) kwa kushirikiana na TLSB. Dkt. Ruzegea amesema maktaba ni kitovu cha maarifa, hivyo rasilimali za elimu kutoka fani mbalimbali hukusanywa ili kuwawezesha vijana kupata taarifa sahihi pamoja na fursa za kugundua na kukuza vipaji vyao. Aliwahimiza vijana kufika maktaba na kutumia huduma za kisasa zinazotolewa ili kuongeza ujuzi unaohitajika katika dunia ya sasa yenye mabadiliko ya kasi ya kiteknolojia. Aidha, amewataka waandishi wa vitabu kuendelea kuzalisha kazi bora zinazoendana na mabadiliko ya teknolojia, akibainisha kuwa Tanzania ina waandishi wengi wenye uwezo mkubwa na wanaochangia katika kuhifadhi historia na utamaduni wa taifa kupitia machapisho. Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wachapishaji Tanzania (PATA), Bw. Hermes Damian, amesema maonesho ya vitabu yanatoa fursa kwa waandishi kuelezea mawazo, uzoefu na hisia zao mbele ya dunia. Alisisitiza umuhimu wa jamii kukuza utamaduni wa kusoma, ikiwemo familia kuwa na vitabu na kumsomea mtoto angalau kitabu kimoja kwa wiki. Bw. Hermes aliongeza kuwa historia na utambulisho wa Mwafrika umehifadhiwa na kuenezwa kwa kiasi kikubwa kupitia vitabu, hivyo wachapishaji wana jukumu muhimu la kulinda na kuendeleza hazina hiyo ya maarifa. Amesema maonesho ya mwaka huu yanatarajiwa kushirikisha nchi mbalimbali duniani pamoja na Jumuiya ya Wachapishaji Afrika (African Publishers Network), hatua inayodhihirisha ushirikiano mpana wa kimataifa katika sekta ya uchapishaji. Naye Katibu wa PATA, Bw. Abdallah Saiwaad, amesema kutakuwepo na mashindano ya usomaji kwa watoto, mabanda ya wachapishaji kutoka ndani na nje ya nchi, pamoja na mauzo ya vitabu kwa bei ya punguzo ili kuongeza upatikanaji wa vitabu kwa wananchi wengi zaidi. Maonesho hayo yatafanyika kuanzia Novemba 21 hadi 26, 2025, yakiongozwa na kaulimbiu: “Vitabu ni Hifadhi ya Maarifa na Utamaduni.”